Mgombea Urais wa UKAWA 2015 Edward Lowassa alianza ziara ya kuingia mitaani Dar es salaam Aug 24 2015 ili kukutana na Wananchi uso kwa uso na kusikiliza matatizo yao.
Lowassa amesema atatusaidia, tuna furaha
sana leo ametutembelea, hatukutarajia,” alisema mwanafunzi wa Shule ya
Nyegulu, Dorcus Wilson baada ya kuzungumza na Lowassa.
Mwanafunzi
mwingine wa Shule ya Msingi Maarifa, Grey Issa alisema amefurahi
kumuona Lowassa kwa sababu amekuwa akimwona kwenye televisheni. Alisema
kero yao kubwa ni unyanyasaji wanaoupata kutoka kwa makondakta wa
daladala.
Baadhi ya wananchi walisema Lowassa ndiye rais wao
mtarajiwa kwa sababu haijawahi kutokea kwa kiongozi yeyote mkubwa kufika
kwenye makazi yao na kuzungumza nao...
“Lowassa ndiye rais wetu. Ni mtu muhimu
sana, amefika kwetu na kuzungumza na sisi. Angekuwa ni kiongozi mwingine
angefika hapa na walinzi wengi,” alisema Augustino Nyembo, mkazi wa
Gongo la Mboto.
Ilipotimu saa 2.35 asubuhi, waziri mkuu huyo wa
zamani, aliingia kwenye daladala lililofika kituoni hapo kupakia abiria
na kusafiri nalo kwenda Chanika. Baadhi ya abiria walistaajabu kumuona
akiingia kwenye daladala hilo na baadhi yao waliteremka kwa mshangao.
Ndani
ya daladala hilo, Lowassa aliketi kiti kimoja na mwanafunzi na muda wa
kulipa nauli ulipofika, kondakta alisema; “Kwa kuwa wewe ni rais
mtarajiwa sitakutoza nauli, utapanda bure”, ombi ambalo mgombea huyo
alilikataa.
Lowassa alitoa noti ya Sh2,000 na kumtaka konda
achukue nauli yake, pia akate ya mwanafunzi aliyekaa naye. Kondakta
alichukua fedha hizo na hakurejesha chenji ya Sh1,400 wala kudaiwa. Watu
wengine waliokuwa wameongozana naye katika daladala hilo walijilipia
nauli ya Sh400 kila mmoja kutoka Gongo la Mboto mpaka Chanika.
Kondakta
huyo, alimweleza Lowassa kuwa tatizo kubwa wanalolipata katika kazi yao
ni kutokuwa na mikataba ya kazi na kwamba wanaweza kufukuzwa muda
wowote bila kuwa na utetezi wa namna yoyote.
Mgombea huyo wa
urais, pia alizungumza na wananchi eneo la Chanika na kuwasikiliza kisha
kuendelea na ziara yake kuelekea Mbagala kwa kutumia gari lake.
Bodaboda wajiunga na msafara
Wakati
msafara wa Lowassa ukielekea Mbagala, baadhi ya waendesha bodaboda
waliufuata hadi uliposimama kwa ajili ya kujaza mafuta eneo la
Kajiungeni.
Mmoja wa vijana hao, Zawadi Mrutu alisema wanampenda
mgombea huyo kwa sababu ni mchapakazi na anaweza kuleta mabadiliko.
Alisema hawajapewa fedha kujiunga na msafara wa Lowassa, bali ni mapenzi
yao.
Alisema kiongozi wa wajasiriamali hao aliyezungumza juzi
kwenye mkutano wa CCM hajui shida wanazozipata barabarani kwani kama
angezifahamu... “asingezungumza vile. Hatumtaki tena kwenye chama
chetu.”
Kijana mwingine, Ali Kasembo alisema wanachotaka ni
mazingira mazuri ya kufanya kazi yao ya kusafirisha abiria. Alisema
wamekuwa wakinyanyaswa na askari polisi katika kazi yao kwa madai kwamba
wanakiuka taratibu.
“Lowassa ni jembe, namkubali sana. Tunataka
atusaidie kupata mazingira mazuri ya kazi ili na sisi tuliojiajiri kwa
kazi hii tujisikie huru, siyo kila siku tunakimbizana na polisi,”
alisema Kasembo, anayefanya shughuli zake za bodaboda Chanika.
Akiwa Mbagala
Msafara
wa Lowassa ulipofika eneo la Rangitatu, Mbagala na wananchi kumbaini,
walianza kufuata gari lake huku wakiimba; “pisha, pisha, Rais apite…,
pisha, pisha, Lowassa apite…”
Ilipotimu saa 4.05 asubuhi,
msafara huo uliingia kwenye Kituo cha Daladala Mbagala Rangi Tatu huku
watu wakisukumana kutaka kumuona.
Hata hivyo, Lowassa alipojaribu kuzungumza nao hakusikika kutokana na kelele zilizotawala kituoni hapo.
Baada
ya spika kufungwa kwenye gari, mgombea mwenza, Juma Duni Haji alisimama
na kusema wamepita kuwasalimia wale ambao wameitwa malofa. Alisema
hatazungumza zaidi kwa sababu wataambiwa walifanya mkutano usiotambulika
rasmi.
“Leo tumepita kuwasalimia maskini wanaoambiwa ni vibaka,
malofa, wapumbavu. Tunaomba mtuache tuendelee na safari, tutakutana
Jumamosi,” alisema Duni na kurejea kwenye gari na kuendelea na safari
yao.
Mwenyekiti Monduli ahamia Chadema
Wakati huohuo; Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Monduli, Arusha, Reuben Ole Kuney ametangaza kujiondoa CCM na kujiunga na Chadema.
Ole
Kuney ambaye aliwahi kuwa mkuu wa wilaya mbalimbali kabla ya kustaafu,
alisema amejiondoa CCM kutokana na kubaini chama hicho kimeshindwa
kusimamia taratibu na kanuni zake.
“Mimi kama mwenyekiti wa
wilaya anayotoka Lowassa, waziri mkuu wa zamani na mbunge wetu, siwezi
kubaki CCM kwani chama kilishindwa kutenda haki katika mambo mengi
ikiwamo mchakato wa urais,” alisema.
Katibu wa CCM wa wilaya
hiyo, Elisante Kimaro alisema kamati ya siasa ya chama hicho itakutana
Jumatatu kujadili mwenendo wake na kupanga ratiba ya kampeni.
Jumanne, 25 Agosti 2015
Tagged Under:
Edward Lowassa alivyoingia mitaani Dar es salaam
By:
Unknown
On: Jumanne, Agosti 25, 2015
Jisajili kwenye:
Chapisha Maoni (Atom)
0 maoni:
Chapisha Maoni