MLINDA mlango wa zamani wa klabu
ya Dar es salaam Young Africans (Yanga SC) ambaye kwa sasa anakipiga
kunako ligi kuu ya nchini Oman (Omantell Professional League) ndani ya
Al Seeb Club, Juma Mpongo huenda akalamba shavu la kusakata kabumbu
katika ligi kuu ya India.
Akizungumza na Shaffihdauda.com
akiwa Oman, Mpongo ambaye amewahi kuzichezea timu za Tanzania prisons,
Twiga sports, Coastal Union na Ashanti United, amesema kuwa mchakato wa
kutimkia India upo kwenye njia na hiyo imekuja baada ya kuwepo na fununu
za kutaka kuzuia magolikipa kutoka nje ya Oman kucheza ligi za nchi
hiyo.
“Kwa kiasi flani naweza sema
ndoto zangu zimetimia, lakini bado nina ndoto ya kupata challenge
nyingine, Pia bado napambana ili niende mbele zaidi kadiri Mungu
atakavyo niwezesha, Kama mipango inaenda vizuri naweza kuhamia ligi kuu
ya India, Mipango inaendelea kaka, bado sijaambiwa ni Timu gani kwa
sasa, Hapa inawezekana sheria zikabadirika baada ya msimu huu
kumalizika, Kuna tetesi msimu ujao wanaweza kufuta kuingiza Magolikipa
kutoka nje ya nchi hii” Amesema Juma Mpongo ambaye timu yake ya mwisho
kuichezea Tanzania ni Ashanti United iliposhuka daraja mwaka jana.
Mpongo ambaye pia amewahi kucheza
soka la kulipwa nchini Congo kunako klabu ya DC Virunga, na Rwanda
katika timu za Kiyovu sports na Rayon sports, amezungumzia kwa ujumla
Maisha ya mpira Oman na tofauti iliyopo kati ya Soka la Tanzania na kwa
waarabu hao ambapo ametililika kama hivi.
“Maisha ya huku sio mepesi sana
kama ambavyo tunafikiria japo ugumu upo tena mkubwa tu, Tofauti kwenye
soka sio kubwa Sana, Lakini huku wenzetu kila kitu wanacho pia kuna
mashindano Mengi ambayo yanamfanya mchezaji awe bize muda wote, Ligi
inaushindani Mkubwa sana, huwezi amini kaka, sisi tumecheza mechi 6
ndani ya siku 11 mashindano tofauti” Amesema Mpongo ambaye timu yake ya
Al Seeb inashika nafasi ya 10 katika msimamo wa ligi ikiwa na pointi 13
huku kinara wa ligi hiyo akiwa na alama 32.
Alituaje Oman?
Kipa huyo ambaye ni mzaliwa wa
Nzega mkoani Tabora, ametoboa siri ya kupata nafasi ya kukipiga Oman na
kusema kuwa, mlinda mlango wa zamani wa Yanga na Taifa Stars, Peter
Manyika ambaye ndio mwalimu wake aliyekuwa akimnoa katika kituo chake
cha makipa kilichopo Karume Jijini Dar es salaam, baada ya kuridhishwa
na kiwango chake akaamua kumpatia ulaji huo na kuwaacha wakongwe kama
Juma Kaseja akibakia Tanzania.
“Kwa kweli nafasi hii nilipewa na
aliyekuwa kocha wa Makiipa wa Timu hii msimu uliopita, Coach Peter
Manyika, Aliona uwezo wangu kwani nilikuwa nafanya mazoezi katika kituo
anachokiendesha hapo Dar uwanja wa Karume ndipo akavutiwa na mimi, Ni
kweli tulikuwa wote pale kituoni mimi, Kaseja na wengineo na wao bado
wanaendelea” Amesema Juma Mpongo ambaye unaweza kumuita Baba Halidi.
Kuhusu familia yake, Je, anaishi nayo Oman?
Mlinda mlango huyo namba moja wa
klabu ya Al Seeb, amesema kuwa licha kuwa na majukumu ya kuhakikisha
analinda lango la timu yake isivamiwe na wapinzani, lakini bado
anamajukumu ya kulea familia yake ya Watoto watatu, pamoja na mke mmoja,
licha ya kuwa mbali nao akimaanisha kuwa Familia yake ipo Dar es
salaam.
“Familia yangu ipo Dar es salaam
kaka, Namshukuru Mungu Nina Watoto watatu wote wakiume, Wa kwanza
anaitwa Halidi Juma Mpongo huyu ana umri wa Miaka 10 sasa, Wa pili
anaitwa Mohamed Juma Mpongo ana umri wa miaka 7 sasa na Wa tatu ambaye
Ndio mdogo anaitwa Rahim Juma Mpongo ana umri wa Miaka 5, Wote wa
napenda Sana soka ila huyu mdogo yeye huwa anataka hadi gloves zangu
nimpe” Amefunguka Juma Mpongo.
Kuna Watanzania wengine wanao cheza Oman?
“Kwenye ligi kuu ni Mimi peke
yangu ila madaraja ya chini yupo Thomas moris ila sijajua anacheza Timu
gani na daraja gani kwani Timu yao ipo nje kabisa ya Muscat” Amesema
Baba Halidi.
Ushauri wake kwa wachezaji na TFF
“Cha msingi ni kujituma na
kufanya kazi kwa bidii kwa Magolikipa mwenzangu, pia TFF na wadau wote
wa soka tupambane ili kuinua soka la nchi yetu maana bado tuko chini, na
ligi yetu iendeshwe kwa msingi ya haki zaidi ili bingwa anaepatikana
aweze kutuwakilisha vizuri kimataifa, TFF iandae mashindano mengine ili
wachezaji wasiwe wanakaa muda mrefu bila kucheza, kuwepo na vikombe, kwa
mfano hapa Oman, kuna kumbe linaitwa Mazda cup Hili limeandaliwa kwa
ajili ya kufanya wachezaji wasikae muda mrefu bila kucheza pindi Timu ya
taifa inapokuwa na majukumu ya Kimataifa, Hayo Ndio maono yangu kaka”
Amefunga kazi mtu mzima Baba Rahim.
0 maoni:
Chapisha Maoni